Wapiga kura 152,147 kuamua uchaguzi Hai

By Godfrey Mushi , Nipashe
Published at 03:52 PM Oct 27 2025
Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Aidan Angetile.

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza idadi ya wapiga kura, 152,147 katika Jimbo la Hai, mkoani Kilimanjaro, watakaoamua kura za Rais, Wabunge na Madiwani Oktoba 29 mwaka huu.

Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Aidan Angetile, amesema maandalizi yote ya uchaguzi huo yamekamilika kwa asilimia 98.

Akizungumza leo (Oktoba 27, 2025), Angetile, amesema kuwa wapiga kura hao wanatarajiwa kushiriki katika uchaguzi huo katika vituo 406 vilivyopangwa katika kata 17.

Aidha, amebainisha kuwa vifaa vyote vya uchaguzi vimepokelewa na kukaguliwa, huku akisema kuwa zoezi la usambazaji wa vifaa hivyo litaanza Jumanne ya Oktoba 28, kuelekea kwenye kata mbalimbali.

Kuhusu wagombea, Angetile, amesema kuwa jumla ya wagombea Udiwani 35 kutoka katika vyama vitano vya siasa watashiriki uchaguzi katika kata hizo.

Kwa upande wa kiti cha Ubunge, msimamizi huyo amesema vyama vitakavyoshiriki ni Chama cha Mapinduzi (CCM), Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia Makini.

Pamoja na mambo mengine, amefafanua kuwa zoezi la kuwafundisha makarani, wasimamizi wa vituo pamoja na wasimamizi wasaidizi limekamilika, na maandalizi ya vituo vyote vya kupigia kura yako tayari kwa ajili ya siku ya uchaguzi.