Kikwete apongeza TAKUKURU kuokoa mil 8/- ujenzi

By Julieth Mkireri , Nipashe Jumapili
Published at 03:29 PM Jan 25 2026
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete akizungumza wakati wa uzinduzi wa jengo la TAKUKURU Chalinze
Picha: Julieth Mkireri
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete akizungumza wakati wa uzinduzi wa jengo la TAKUKURU Chalinze

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amezindua jengo jipya la Ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Chalinze, huku akiwapongeza kwa kuonyesha uzalendo wa kuokoa Sh. milioni nane katika fedha za ujenzi zilizotengwa na kutumika Sh. milioni 406.4 kati ya 414.6 zilizotengwa.

Amesema kilichofanywa na taasisi hiyo ni funzo kwa wengine huku aksisitiza kwamba, serikali itaendelea kuwa wakali kuhakikisha fedha zinazotengwa zinatumika kama zilivyopangwa na miradi inakamilika kwa kiwango kinachotakiwa.

Vilevile amewataka watendaji wa taasisi za umma nchini kutoa kipaumbele kwa wakandarasi wa maeneo husika pindi wanapotekeleza miradi ya serikali, huku akisema hatua hiyo itachochea maendeleo ya wananchi katika maeneo yanapotekelezwa miradi hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Chalamila, amesema mradi huo ambao umetekelezwa na ofisi ya TAKUKURU Chalinze, ulianza Mei, 2024 na ulikabidhiwa Januari, 2025 ukiwa umekamilika.

Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Chalamila
Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, amesema mafanikio makubwa waliyoyapata kwenye eneo la uwekezaji, yametokana na kazi inayofanywa na TAKUKURU.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, akiongoza viongozi wengine uzinduzi wa jengo la TAKUKURU Chalinze
Ameipongeza TAKUKURU kwa mchango wake katika kuimarisha mazingira wezeshi ya uwekezaji mkoani humo, kupitia kudhibiti rushwa na kupunguza urasimu.

Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Pwani, Domina Mkama, amesema jengo lililokuwa linatumika awali ambalo ni la kukodi, walishindwa kuweka miundombinu ya mawasiliano, huku wananchi wakishindwa kuwafikia kutokana na eneo waliko.

Mkama amesema jengo hilo jipya lina mazingira rafiki ya wananchi kutoa taarifa tofauti na la awali, ambalo wengi walikosa uhuru wa kuifikia taasisi hiyo.